Tuesday 11 June 2013

Maalim Seif aikosoa Rasimu ya Katiba Mpya

Zanzibar. Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad amesema hajaridhishwa na rasimu ya kwanza iliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyoongozwa na Jaji Joseph Warioba.
Kauli hiyo aliitoa wakati akihutubia maelfu ya wafuasi wa chama chake katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Tundangaya Matemwe iliyoko Wilaya Kaskazini ”A’ Unguja.
Alisema chama chake kimeunda jopo la wanasheria weledi kwa lengo la kuipitia na kuichambua kifungu baada ya kifungu ili kutoa ushauri kuhusu rasimu hiyo.
“Rasimu hiyo mimi sikuridhika nayo tumeiona na tumeipitia na tumeunda jopo la wanasheria ili watushauri,” alisema Maalim Seif huku akishangiliwa na wanachama wake.
Alibainisha kuwa kuna mambo ambayo yalitakiwa yatolewe katika mambo ya Muungano ndani ya rasimu hiyo ambayo yangetoa mamlaka kamili ya Zanzibar bado yamebakishwa yakiwa ni mambo ya Muungano.
Mambo hayo ni kama ulinzi na usalama, sarafu na Benki Kuu, mambo ya nje ,usajili wa vyama vya siasa ushuru wa forodha na mapato yasio ya kodi yatokanayo na mambo ya muungano
Alisema kwa Zanzibar kwa yale mambo ambayo si ya Muungano wataweza kushirikiana na nchi yoyote ile duniani.
Alisema kuna baadhi ya mambo walitaka kuwamo ndani ya rasimu ya Katiba Mpya kuna baadhi ya mambo hayo yamo na mengine hayamo kabisa lakini mengine hayamo na mengine yamo nusu.
Hata hivo akizungumzia suala la kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura alisema ili uweze kutoa uamuzi wa nchi yako lazima uwemo katika daftari la wapiga kura la Wazanzibari kama humo huwezi kupiga kura.
Alimtaka Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi, Jecha Bakari Jecha kuwa tume yake ni mpya tayari imepanga mikakati ya kuwakosesha wananchi kujiandikisha kwa kutumia mawakala au sheha akimkataa tu mtu basi asiandikishwe.

No comments:

Post a Comment